
MKUTANO wa Rais Jakaya Kikwete na viongozi wa juu wa vyama vya siasa uliofanyika jana mjini Dodoma umetajwa kuwa na dalili nzuri zinazoashiria mwafaka utapatikana juu ya mchakato wa utengenezaji
Katiba
mpya. Kikwete alikutana jana na vyama hivyo kupitia Kituo cha Demokrasia
Tanzania (TCD) kinachoongozwa na Mwenyekiti wa UDP, John Cheyo kukiwa na ajenda
mbili mojawapo ikihusu mchakato unaoendelea wa kutengeneza Katiba mpya.
TCD
inaundwa na vyama vyenye uwakilishi bungeni, ambavyo ni CCM, CUF, CHADEMA, TLP,
NCCR-Mageuzi na UDP. Ingawa
yaliyojiri
ndani ya mkutano huo unaotajwa ulijaa amani na ucheshi hayakuwekwa wazi, Cheyo
ambaye ni Mwenyekiti wa TCD alisema ajenda nyingine ilihusu Uchaguzi Mkuu wa mwaka
2015.
Akizungumza
na mwandishi wa habari hizi, Cheyo alisema mkutano huo ulienda vizuri na
wamekubaliana Septemba 8, mwaka huu, kukutana kwa mazungumzo zaidi ambayo
anaamini kutakuwa na matokeo chanya.
“Mkutano
umeenda vizuri sana…ulikuwa mkutano mzuri sana, ulijaa amani na ucheshi.
Tumekubaliana kwamba tunakutana tarehe 8, Septemba,” alisema Cheyo.
Akielezea
imani yake juu ya mkutano huo wa wiki ijayo katika suala zima la kupata mwafaka
juu ya mchakato wa Katiba mpya, baada ya Kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi
(Ukawa) kususa, Cheyo alisema, “…kukubaliana kukutana tu, ni jambo muhimu sana
na lenye dalili nzuri.”
Kwa
mujibu wa Cheyo, mkutano huo ulitawaliwa na utulivu, ucheshi jambo ambalo
anaamini utamaduni wa Watanzania wa kukaa na kuzungumza utazaa matunda katika
mkutano ujao.
Cheyo
ambaye alishiriki pamoja na Katibu wa chama chake, Isack Cheyo, alisema
wanachama wote wa TCD akiwemo mwakilishi wa vyama visivyo na wabunge,
walihudhuria na kushiriki mkutano huo kwa ufasaha.
Kwa
upande wa CCM, walioshiriki ni Makamu Mwenyekiti Bara, Philip Mangula na Katibu
Mkuu, Abdulrahman Kinana. Chadema aliyeshiriki ni Katibu Mkuu wake, Dk Wilbrod
Slaa pamoja na Mwanasheria wa chama hicho, Tundu Lissu.
Washiriki
wengine ni Mwenyekiti wa Chama cha NCCR Mageuzi, James Mbatia na Katibu Mkuu
wake, Mosena Nyambabe.
CUF
iliwakilishwa na Mwenyekiti wake, Profesa Ibrahim Lipumba na Naibu Katibu Mkuu
Bara, Magdalena Sakaya.
Kwa
upande wa TLP, Mwenyekiti wake, Augustino Mrema na Katibu Mkuu wake, Jeremiah
Shelukindo walishiriki.
Aidha
Mwenyekiti wa United Peoples Democratic Party (UPDP), Fahmi Dovutwa
aliwakilisha vyama visivyo na wabunge katika
TCD.
Cheyo alisema kabla ya mkutano huo wa wiki ijayo, Septemba 6 na 7, TCD itakuwa
na mkutano wake mkuu utakaokutanisha wanachama kabla ya kesho yake kukutana na
Rais.
Ajenda
kuhusu mchakato wa Katiba mpya, unazingatia hali ya sasa ya kisiasa ambayo,
kundi la Ukawa lilisusa Bunge Maalumu la Katiba kwa madai ya kutoridhishwa na
mwenendo wake.
Tangu
Ukawa wasuse Bunge hilo linaloendelea mjini Dodoma, wananchi na makundi
mbalimbali ya kijamii yamekuwa yakitaka wajumbe hao waliosusa warejee bungeni
kuungana na wenzao waliobaki kutengeneza Katiba yenye maridhiano.
Licha
ya kuwepo sauti za kusihi kundi hilo kurejea bungeni, pia wapo ambao wamekuwa
wakisisitiza maridhiano kati ya Ukawana Tanzania Kwanza yapatikane ili kuunda
Katiba yenye ushiriki wa makundi yote.
Wadau
wengine, likiwemo Jukwaa la Wakristo Tanzania lililotoa taarifa yake jana
kuhusu mchakato wa Katiba, na kumwomba
Rais
Kikwete asitishe Bunge hilo ili upatikane mwafaka na maridhiano.Katika taarifa
ya jukwaa hilo linalojumuisha Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) Baraza la
Makanisa ya Pentekoste (CPCT),
Jumuiya
ya Kikristo Tanzania (CCT) na Kanisa la Waadventista Wasabato, limeomba
mchakato uahirishwe kuepusha athari kwa mshikamano na umoja wa taifa.
Mjadala
bungeni kesho BUNGE Maalumu la Katiba litaanza majadiliano kesho baada kamati
zote kumaliza kupitia na kuchambua sura zote za Rasimu ya Katiba. Jana na leo
kwa mujibu wa Katibu wa Bunge hilo, Yahya Hamad kamati hizo ilikuwa ziwasilishe
taarifa zao kwa Sekretarieti ya Bunge ambayo itaanza kuzichambua kabla ya
kuzipeleka kwenye Bunge.
Hamad
alisema licha ya kuzichambua, Kamati ya Uongozi itakutana leo kwa ajili ya
kujadiliana mambo mbalimbali kabla ya majadiliano kuanza kesho.
"Ratiba
yetu inaonesha kuwa Jumanne (kesho) Bunge lote litakutana kwa ajili ya
majadiliano ambayo ni muhimu sana ili kuwekana sawa," alisema Hamad.
Alisema siku 15 zimepangwa kwa ajili ya majadiliano ili taarifa hizo pamoja na
maoni ya wajumbe wakati wa mjadala yawasilishwe kwa Kamati ya Uandishi wa
Rasimu ya Katiba.
Hamad
alisema Bunge hilo likishakamilisha mjadala, ndipo Kamati ya Uandishi wa Katiba
ambayo iko chini ya Mwanasheria maarufu Andrew Chenge itaanza kazi ya kuandika
Rasimu ya Katiba.
Alisema
Kamati ya Chenge pia italazimika kurejesha Rasimu hiyo ndani ya Bunge kuona
kile walichokiandika ni sahihi kabla ya kupigiwa kura na wajumbe wote. Bunge
hilo limehitimisha siku 30 ambazo walizitumia kwa kamati mbalimbali kujadili
Rasimu ya Pili ya Katiba iliyowasilishwa bungeni hapo na Mwenyekiti wa Tume ya
Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba.
Kwenye
majadiliano hayo, kamati mbalimbali zilitupilia mbali baadhi ya mapendekezo
yaliyoko kwenye Rasimu ya Katiba ikiwemo lile linalotaka wabunge wawe na ukomo
na wananchi kupewa haki ya kumwondoa mbunge wao madarakani.
Eneo
lingine ambalo baadhi ya kamati ziliyakataa ni ambayo yalitaka baadhi ya
wateule wa Rais kutakiwa kuthibitishwa na Bunge kwa maelezo kuwa viongozi
wanaotakiwa kuthibitishwa na chombo hicho, ni wale tu wanaowajibika kwa Bunge
hilo.
Lakini
pia kuna mvutano wa aina ya Bunge litakaloundwa kutokana na baadhi ya wajumbe
kutaka mambo ya Tanzania Bara yajadiliwe na Watanzania Bara tu na pia yawepo
mambo ya Muungano ambayo yatajadiliwa na wabunge kutoka pande zote za Muungano.
Hoja
ya uraia pacha pamoja na suala la Kadhi Mkuu nalo ni miongoni mwa yanayodaiwa
kukabiliwa na mvutano ndani ya baadhi ya kamati.
Source:Habari Leo
No comments:
Post a Comment