Sunday, May 18, 2014

Mwanafunzi wa kidato cha pili mbaroni kwa kukutwa na silaha Manyara



JESHI la Polisi mkoani Manyara, linawashikilia watu watano kwa makosa tofauti, likiwemo la Mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule ya Sekondari Chief Sarwati, akiwa na Bastola moja aina ya Chines iliyofutwa namba za usajili pamoja na risasi 6 zikiwa ndani ya magazine kinyume cha sheria imeelezwa. 
Akithibitisha kutokea kwa matukio hayo leo Mei 16, 2014, Kamanda wa Polisi mkoani humo, Deusdedit Nsimeki, amesema katika tukio la kwanza lilitokea Mei 14,2014 ambapo Polisi walimkamata, Said Shabani (16) mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule hiyo, na Lutemba John (22) mkazi wa mkoa wa Kigoma wakiwa na silaha hiyo kinyume na sheria.
 
Nsimeki, amesema kuwa watuhumiwa hao kwa pamoja walikamatwa kwenye gari namba T. 313 ALZ, Rosa mali ya Laurent Sule, ambapo gari hilo hutumika kusafirisha abiria toka Mbulu kwenda Hydom.
“Hawa tutaendelea nao kwa mahojiano kuhusiana na hiyo Bastola na risasi husika na kujua walikuwa wanaenda wapi, kwani kutokana na taarifa za awali zinasema kwamba walikuwa wanaenda kufanya ujambazi huko Hydom” alisema Nsimeki.
Wakamatwa wakivua samaki na kutoroka mikononi mwa Polisi
Amesema katika tukio lingine lilitokea Mei 15, 2014 saa tisa alfajiri maeneo ya Himiti, ambapo wananchi wapatao 30 wakiongozwa na Mwenyekiti wa kijiji hicho, Idd Hassan, (53) wakiwa kwenye msako waliwakamata watu wanaovua samaki ndani ya Ziwa Babati kwa kutumia sumu, wakati ziwa hilo likiwa limefungwa na Serikali ya mkoa.
“Ilipofika muda huo, wananchi kwa kushirikiana na mwenyekiti huyo pamoja na Askari Polisi, tulifanikiwa kukamata watu watatu ambao walikuwa wanafanya shughuli hiyo katika Ziwa Babati kinyume na taratibu na sheria, alisema Nsimeki. Amewataja watuhumiwa hao kuwa ni, Athuman Rashid (32), Halifa Hussein (28), na Hassan Hamis (33) ambao kabla ya kufikishwa ufukweni walijirusha Kwenye Ziwa hilo na kufanikiwa kutoroka.
Amesema katika msako huo, waliweza kukamata samaki kilo 60, nyavu moja pamokja na dawa aina ya DAZBAN iliyotumika kuua/kuvua samaki hao, ambapo kwa mujibu wa taarifa hiyo inasadikiwa dawa hiyo kwenye maduka ya pembejeo za kilimo.
Walipuliwa na baruti ndani ya mgodi Simanjiro
Wakati huo huo, amesema Mei 5, 2014 saa moja jioni katika eneo la Kitalu D kwenye mgodi namba PML 00089 Wilaya ya Simanjiro mkoani humo, wafanyakazi watatu, Abdalla Mohamed (40), mkazi wa Songambele, alijeruhiwa usoni na kukatika mkono wake wa kulia, Hussein Haji (34), mkazi wa Songambele aliumia usoni na mkono wa kulia na Mudi Mohamed (36), mkazi wa Zaire kati, ambaye alijeruhiwa usoni, kwa pamoja walilipukiwa na baruti wakati walipokuwa wakifanya kazi chini mgodini.
“Majeruhi walipelekwa Hospitali ya Mkoaranga iliyopo Wilaya ya Arumeru mkoa wa Arusha kwa matibabu na mpaka sasa hatujapokea taarifa yoyote ile ambayo inasema labda wamefariki, bali bado wanaendelea na matibabu na sisi tunaendelea na uchunguzi wa tukio hili ili kujua kama kulikuwa na uzembe ili kuchukua hatua za kisheria” alisema Nsimeki.
 Source: jamii forum

No comments:

Post a Comment