Friday, September 5, 2014

SIFA YA KIDATO CHA NNE KUWA MBUNGE SASA YAPINGWA.



 
KAMATI nyingi za Bunge Maalumu la Katiba, zimekataa sifa ya elimu ya kidato cha nne, kuwa kigezo cha msingi cha mgombea ubunge, kwa madai kuwa inabagua wananchi kwa kuondoa haki yao ya kidemokrasia ya kuomba kupigiwa kura na kupiga kura.
Hata hivyo, kamati hizo zimeweka sifa ya kuwa mbunge, iwe ni kujua kusoma na kuandika, bila kufafanua kama sifa hiyo nayo, inaweza kuleta ubaguzi huo.
Ibara ya 26 kifungu cha kwanza cha rasimu ya Katiba, kinaeleza kuwa sifa ya kugombea ubunge ni kujua kusoma na kuandika, lugha ya Kiswahili na Kiingeza na ana elimu isiyopungua kidato cha nne.
Lakini taarifa za kamati nyingi zimeeleza kuwa suala la kugombea nafasi yoyote ni la kidemokrasia, haipaswi mtu kuzuiwa kugombea kwa kigezo cha elimu, kwani hii ni haki ya kikatiba.
Katiba haitakiwi kuweka kigezo chochote kinachokiuka haki za msingi za kuchaguliwa au kuchagua,” ilisema taarifa namba 10 ya Bunge hilo. Kamati hiyo pia ilisema haki ya kuamua kama mgombea anafaa au hafai ni ya wapiga kura, wasizuiwe kikatiba kutumia haki yao ya msingi ya kuchagua mtu wanayemtaka.
Walisema utaratibu huo haupo duniani kote hata nchi zilizokomaa na demokrasia iliyokomaa.
Ni kamati namba mbili tu, ndio ambayo imetaka sifa ya mtu kuwa mbunge iwe elimu ya kidato cha nne, lakini pia awe ni raia wa kuzaliwa na hana uraia wa nchi nyingine na aliyetimiza umri wa miaka 21.
Kuhusu watu ambao waliwahi kukutwa na makosa ya jinai kutogombea, baadhi ya kamati zinapendekeza kuwa makosa hayo yawe ya ubakaji au ujangili, ili kutowakataza waliohukumiwa kwa makosa madogo madogo ya jinai na kunyimwa fursa ya kugombea nafasi ya ubunge.
Wajumbe hao pia wametaka ibara ya pili (a) inayozungumzia muda wa ukomo wa ubunge wa vipindi vitatu, ifutwe ili kuwapa fursa wabunge ambao ni watendaji wazuri katika maeneo yao, kuendelea kugombea na kuchaguliwa na wananchi kwa sababu kimsingi ni haki ya mtu kikatiba.
Pia walisema hiyo itawapa uhuru wananchi kuchagua mbunge wanayemtaka, hata kama ameshashika madaraka hayo kwa vipindi vitatu mfululizo.
Hata hivyo wametofautiana katika eneo la watumishi wa umma wanapoamua kugombea ubunge, urais na udiwani makamu wa rais au nafasi nyingine katika chama cha siasa, wapo wanataka mtu huyo utumishi wake ukome pale anapogombea, lakini wapo wanaotaka mtumishi huyo ahesabiwe kama yuko likizo bila malipo.
Kwa upande wa uongozi wa Bunge, karibia kamati zote zimekubaliana na rasimu ya Tume ya Marekebisho ya Katiba ambayo yanataka mbunge, waziri, naibu waziri wasiruhusiwe kugombea uspika wala unaibu uspika.
Sababu za kukubaliana na hoja hiyo ni kwamba ni kutoa uhuru kwa spika na naibu wake kufanya kazi yake kwa uhuru bila kuingiliwa na chama chake cha siasa.

No comments:

Post a Comment