Thursday, August 14, 2014

PHIRI SASA AAHIDI UBINGWA SIMBA SC.

Kocha mpya wa Simba, Patrick Phiri akiwapungia mashabiki waliofika kumlaki kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam jana baada ya kutua nchini kuanza kazi ya kuifundisha timu hiyo kwa mara ya tatu. (Picha na Cosmas Mlekani).
KOCHA mpya wa Simba, Patrick Phiri ametua jana Dar es Salaam na kuahidi kurudisha heshima ya Simba.
Kocha huyo raia wa Zambia, alitua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), saa 7:30 mchana na kupokewa na wajumbe watatu wa Kamati ya Utendaji, Said Tully, Collin Frisch na Idd Kajuna pamoja na baadhi ya mashabiki waliokuja kumlaki.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kutoka nje ya uwanja huo, Phiri alisema anamshukuru Rais wa Klabu ya Simba, Evans Aveva kwa kumpa kazi na kuahidi kurudisha ubingwa.
“Tanzania ni nyumbani kwangu kwa pili, nashukuru kurudi tena katika klabu hii, nitajitahidi kufanya kazi kwa bidii na kuleta heshima,” alisema Phiri.
Mzambia huyo aliyewahi kuinoa Simba kwa vipindi viwili tofauti, anakuja kurithi mikoba ya Zdravko Logarusic, raia wa Croatia, aliyefukuzwa Jumapili.
Phiri alisema alikuwa akiifuatilia timu kwa muda mrefu kwani imekuwa na matatizo, lakini sasa, baada ya kurudi anaamini mambo yatakuwa mazuri msimu ujao.
“Simba ilikuwa ina matatizo kwa muda mrefu, nitayaondoa kwa sababu naijua klabu hii vizuri,” alisema na kuwashukuru mashabiki na wote waliofika kumpokea kwenye uwanja huo wa ndege.
Hata hivyo, chanzo kimoja cha Simba kilisema kuwa huenda akasaini mkataba wa miaka miwili. Kuja kwake katika klabu hiyo ni kwa mara ya tatu, ikiwa alikuja kwa mara ya kwanza msimu wa 2003 hadi 2005 na baadaye mwaka 2006 hadi 2008.

Phiri aliiongoza Simba kunyakua ubingwa na kumaliza msimu wa mwisho bila kupoteza mechi hata moja.

1 comment: